MGOGORO WA AZANIA NA TAMBAZA XXXVI

 

Adeladius Makwega-DODOMA

Msomaji wangu unaweza ukajiuliza je kwanini Mwanakwetu anamzungumzia wakili Phidelis Mwidunda? Kwa hakika hii nyaraka yangu iliyokwenda katika Bodi ya Rufaa ilitayarishwa na Ndugu Peter Pinda, mheshimiwa sana, katika hatua za kukusanya ushahidi, hilo nina hakika nalo kwa asilimia 100 lakini hata kuandika katika hatua za awali hadi mwisho.



Nina hisi wakati inayatarishwa katika hatua za mwisho ndugu Peter Pinda mheshimiwa sana alimshirikisha wakili Phidelis Mwidunda.

Nina hisi kuwa kumshirikisha huko kulikuwa kwa mawasiliano ya simu tu. Kama mheshimiwa sana asingaliniambia kuipelekea nakala hiyo nisingali fahamu kuwa ndugu huyu alishiriki kuitayarisha nyaraka hiyo.


Ndiyo kusema kwa ukweli wa Mungu, Wakili Mwidunda hakunihoji chochote na wala hakukutana na akina Ibrahimu Liguo, Atanas Luis na Hamisi Ramadhani (Rashidi Kazyoba)Edgar Chibula wille John,Emmanuel Yesaya  na wengine ambao hadi leo hii wapo hai.



Kwa kuwa msomaji wangu katika matini iliyotangulia nimezungumzia kwa kiasi kidogo Wakili huyu wa serikali naomba kwa kiasi nikuume sikio juu ya wakili huyu.



Ndugu huyu alizaliwa katika Kijiji cha Kiwele Kitongoji kinachofahamika kama Mapinduzi Wilaya ya Iringa Vijijini, mkoa wa Iringa kama nilivyofika huko mwaka 2006 nikikusanya taarifa za ndugu huyu.



Ukifika Iringa Mjini ukiwa unaelekea Chuo Kikuu cha Mkwawa kuna njia inaelekea bondeni hiyo njia ndiyo inakwenda huko Mapinduzi-Kiwele na nadhani kisiasa lile ni jimbo Kalenga na siyo Jimbo la Isimani.



Kijiji hiki nilibaini ni cha watu masikini sana huku wakilima kunde, mahindi, tumbaku na hata Mpunga kwa bondeni. Kwa wakati huo walikuwa na shule ya msingi ambayo ndiyo aliyosoma wakili huyu na shule moja mpya ya sekondari, pia wakiwa na zahanati.

Kijiji hiki kikaliwa na Wahehe na Wabena wengi.

 

Umbali kutoka shule ya msingi, sekondari na zahanati ilikuwa kama dakika 20 za mguu kutoka kwenye makazi ya baba wa Wakili Mwidunda.


Ndugu huyu kwa utafiti wangu nilibaini kuwa kidato cha nne na cha sita alifanya vizuri sana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alisoma sheria pia alifanywa vizuri sana, hata Chuo Kikuu cha Malta-Italia ambapo alifanya shahada ya uzamili katika sheria za bahari pia hakukiuka mwiko wake, alifanya vizuri mno.

.

Mahakama ina sifa moja kubwa ya kuhifadhi kumbukumbu ya mashauri makubwa makubwa, miongoni mwa kesi kubwa ambazo ndugu huyu aliiwakilisha serikali vizuri mahakamani ni ile ya rufaa ya mke wa Marehemu Imrani Kombe, ambapo mama huyo aliomba alipwe kiasi fulani cha fedha ambacho kilikuwa kikubwa mno, upande wa serikali uliomba alipwe nadhani milioni 200 kama fidia baada ya mauwaji ya mumewe ili aweze kutunza familia naye mama huyu akiomba milioni 500.

Nadhani ombi hilo la serikali lilikubaliwa na mahakama, wanasheria kama mnasoma matini hii mtanisaidia pale nilipokwenda kombo.

Kwa hiyo rufaa yangu iliandaliwa na wabobezi wa sheria kweli kweli hata ndugu Peter Pinda ni hatari sana kwenye sheria, japokuwa yeye huwa na desturi ya kama kuigiza kuwa yeye si mbonezi (huwa ni mtu wa kujishusha).

Unaweza kusema kesi hii ya Tambaza ilikuwa ni ndogo, mbona Mwanakwetu alitumia nguvu kubwa kuielezea?

Mwanakwetu tambua kuwa kesi ni kesi tu maana maamuzi ya kesi ni mawili kushinda au kushindwa yana athari kubwa katika maisha ya binadamu.

Phidelis Mwidunda kama asingalishiriki katika kutayarisha nyaraka hizi leo hii nisingalimkumbuka kabisa.



Nitoe ushauri kwa rafiki zangu wanasheria wote msidharau kesi yoyote, unayoletewa na mteja wako, ifanyie kazi kwa moyo wote na uwezo wako wote, tambua dunia ina kesho, mambo ya kesho Mungu anajua.

Lakini pia kesi ndogo ya mteja inaweza kukupa mteja mwenye kesi kubwa.

Angaweza kumwambia ndugu Peter kuwa achana nao, hao wanafunzi wa Tambaza ni wahuni tu, wavuta bangi, lakini hawakufanya hivyo.


Kwa bahati mbaya Phidelis Mwidunda leo hii macho yake, masikio na kiwiwili chake kimelala katika makaburi ya huku kwao Mapinduzi-Kiwele mkoani Iringa, maana alifariki mwaka 2003, natambua matini hii inaweza kusomwa na watoto wake, nduguze na Wanyaulukolo wa Iringa Vijijini. Mungu awakabiriki sana.

Kwa leo naiweka chini kalamu yangu hapo.

Mungu ailazee roho ya marehemu Phidelis Mwidunda pahala pema peponi amina.

makwadeladius@gmail.com

0717649257

 

 

 

0/Post a Comment/Comments